Thursday, February 13, 2014

Tamko la wadau wa afya kwa vyombo vya habari juu ya Haki ya Afya na Rasimu ya Katiba mpya: Feb 13, 2014



Kwanza tunapenda kuipongeza Tume ya Katiba kwa kazi kubwa waliyofanya katika kukusanya maoni na kuandaa rasimu ya pili ya Katiba na vilevile kwa kugusia Afya katika Haki za binadamu kwa baadhi ya makundi kama vile katika Haki ya wanawake Ibara ya (47) kifungu cha 1(g) mwanamke ana haki ya kupata huduma bora ya Afya, katika Haki ya  watoto Ibara (43) kifungu cha (1)e kinachosema mtoto ana haki ya kupata lishe bora, huduma ya Afya, makazi na mazingira yanayomjenga kimaadili.

Hata hivyo, tunasikitika kwamba Haki ya Afya haijatambuliwa kwenye rasimu kama haki ya Msingi ya kila mwananchi. Tukiwa kama wadau wa Afya, tunapenda kufafanua kuwa Afya ni kuwa mzima kiakili, kimwili, kijamii, kimaadili na kimazingira, hivyo Afya ni haki ya msingi ya kila mwananchi. Mwananchi anapokosa haki hii ya msingi hushindwa kushiriki katika shughuli mbalimbali za kuleta maendeleo, na kupata madhara mengine yanayoweza kusababisha kifo.

Katika rasimu ya pili ya Katiba iliyokabidhiwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kujadiliwa katika Bunge la Katiba Februari 2014, Afya kama Haki ya msingi ya binadamu haijatambuliwa kama vile haki zingine zilivyotambuliwa kwa mfano elimu.

Tunatambua kwamba Katiba ndiyo sheria Mama, hivyo basi, pasipo kutambua Haki ya Afya, sheria ndogondogo haziwezi kulitambua suala hili nyeti, na hivyo kuiweka jamii na vizazi vijavyo katika hali hatarishi kiafya.

Juni 2013, Sikika iliomba na hatimaye ikapata kibali rasmi kutoka Tume ya mabadiliko ya Katiba cha kutambuliwa kama Baraza la Katiba kwa ajili ya kuchambua na kukusanya maoni juu ya Rasimu ya Katiba. Sikika ilishirikisha wananchi na Asasi mbalimbali kama Tanzania Public Health Association (TPHA), Medical Association of Tanzania (MAT) na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) katika  kuchambua rasimu ya kwanza ya Katiba na hatimaye kutoa mapendekezo ya kutambua haki ya afya kwenye Katiba. Mapendekezo hayo yaliwakilishwa kwa Tume Agosti 2013 lakini hayakuchukuliwa, kwa sababu moja au nyingine.

Kutokana na umuhimu wa Afya kwa kila mwanadamu, tunapendekeza Afya itambulike kama Haki ya msingi katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na iwe ni wajibu wa kila mwananchi kutunza Afya yake, kushiriki na kusimamia masuala yanayohusu afya ya jamii. Pia serikali ya Jamhuri ya Muungano, mamlaka za nchi pamoja na taasisi zihakikishe kuwa Haki hii ya msingi inasimamiwa vyema. Pia itambuliwe kuwa ni kosa la jinai kwa mwananchi kufanya tendo lolote linalohatarisha afya ya mtu mwingine na jamii kwa ujumla.

Pia tunaomba serikali na wadau wa Katiba waangalie na kutambua Afya kama suala la msingi linalotakiwa lizingatiwe katika sera zote za maendeleo ili kuweza kulinda afya ya Watanzania wote.

Aidha, tunapendekeza ibara ya 41 inayozungumzia uhuru na haki ya mazingira safi na salama iongeze masuala haya;  (1) Serikali ihakikishe kuwa kila mwekezaji afanye tathmini ya kiafya kabla mradi haujaanza na utekelezaji wa mapendekezo ushirikishe wadau wote hususan, ngazi ya jamii. (2) Serikali na vyombo husika vidhibiti uingizwaji na utumiaji wa vifaa/vyakula/madawa vyenye viwango duni na pia kutoruhusu matumizi ya madawa au vyakula bila ya ushahidi wa kitafiti unaothibitisha usalama wa mtumiaji/mlaji. Kutompatia mwananchi haki ya afya ni sawa na kumnyima haki ya kuishi kama ilivyoainishwa katika ibara 24 ya rasimu ya Katiba, maana uhai we mtu unategemea afya aliyo nayo.

Tunaamini kwamba bado kuna nafasi ya kuitambua Afya kama Haki ya msingi, hivyo tunatoa wito kwa Wajumbe, Viongozi na Wabunge wazingatie suala hili wakati wa kuijadili rasimu ya Katiba katika Bunge la Katiba.

Tamko hili limeandaliwa kwa ushirikiano kati ya Sikika, Tanzania Public Health Association (TPHA), Medical association of Tanzania na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).



Mkuu wa programu Sikika Josaphat Mshighati (Kushoto), Mwenyekiti wa TPHA Dk. Elihuruma Nangawe,  Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania Dk. Primus Saidia (Katikati) na Mwenyekiti wa kamati ndogo ya katiba TPHA Bi.Grace Mtawala (Kushoto) wakitoa tamko la pamoja juu ya Haki ya Afya na rasimu ya Katiba mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani).
Mkuu wa programu Sikika Josaphat Mshighati akitoa tamko la pamoja juu ya Haki ya Afya na rasimu ya Katiba mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani). Katikati ni Mwenyekiti wa TPHA Dk. Elihuruma Nangawe na Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania Dk. Primus Saidia.
Mwenyekiti wa kamati ndogo ya katiba TPHA Bi Grace Mtawala (Kulia), Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania Dk. Primus Saidia, Mwenyekiti wa TPHA Dk. Elihuruma Nangawe (Katikati) na Mkuu wa programu Sikika Josaphat Mshighati wakitoa tamko la pamoja juu ya Haki ya Afya na rasimu ya Katiba mbele ya waandishi wa habari (hawapo pichani).

No comments: