Ripoti hiyo ilitaja baadhi ya bidhaa zisizokuwa na ubora ambazo zinaweza kuwa katika mzunguko wa soko huku TBS ikiwa ina ufahamu. Baadhi ya bidhaa hizo ni pamoja na vinywaji vya kuongeza nguvu, Siagi, mafuta ya maji ya kupikia, sabuni za aina mbalimbali ikiwa ni pamoja na zile za kuoshea nywele (Shampoos).
Hali hii ni kashfa
kubwa kwa taasisi hizi mbili kubwa nchini zilizopewa dhamana ya
kuwalinda wananchi dhidi ya bidhaa zilizo chini ya ubora. Hii inaonyesha
kwamba taasisi hizi zimeshindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu.
Cha kusikitisha zaidi ni kwamba wizara husika zimeshindwa kuziwajibisha
taasisi hizo.
Sikika
inatoa wito kwa serikali pamoja na wizara husika kutekeleza mapendezo
ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ikiwa ni pamoja na kubadilisa
utawala wa uongozi wa Shirika la viwango Tanzania (TBS). Taarifa ya CAG
iliyowasilishwa kwa kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali Kuu na Kamati
ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma pamoja na kamati ya Bunge ya
Viwanda na Biashara ilitaja thamani ya bidhaa hizo kuwa ni Tsh. 1.8
billioni ambazo zilikuwa chini ya kiwango na ziliweza kuingia sokoni.
Bidhaa hizo zilikuwa zimekaguliwa na TBS na kuonekana hazifai kwa
matumizi ya kawaida na matumizi ya binadamu.
Ripoti
hiyo ya CAG inasema kuwa hata baada ya TBS kuamini kuwa bidhaa hizo
zilikuwa chini ya kiwango, hakuna ushahidi wowote uliotolewa na taasisi
hiyo kuwa bidhaa hizo zilirudishwa nchi zilikotolewa au kwamba
ziliharibiwa. Hii inamaana kuwa bidhaa hizo zimeshaingia sokoni na kwa
bahati mbaya zinaweza kuleta madhara makubwa kwa wananchi
watakaozinunua na kuzitumia.
Ni
kweli kwamba baadhi ya bidhaa hizo zina madhara ya moja kwa moja kwenye
ngozi ya binadamu na kwa zile zinazotumika kama kinywaji zinaweza
kuleta madhara makubwa ya kiafya kwa watumiaji walio wengi. Kwa bidhaa
ambazo hazina kiwango kama vile vinywaji vya kuongeza nguvu, siagi na
mafuta yatokanayo na mbegu za alizeti, kama yana sumu yanaweza
kusababisha mtu kuugua sana na hivyo kusababisha mtu kupoteza maisha. Ni
wazi kabisa kwamba athari kubwa itakayotokana na matumizi ya bidhaa
hizi ni gharama za matibabu kitu ambacho ni sawa na kuongezea serikali
mzigo kwenye kutoa huduma za afya ambazo hata kwa sasa hazitoshelezi.
Hii
sio mara ya kwanza kwa TBS kuhusika katika kafsha kama hii. Mwaka 2011,
kaimu mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma
Bwana Deo Filikunjombe aliishutumu TBS kwa kuidanganya kamati hiyo kuwa
wana ofisi nje ya nchi inayoshughulika na ukaguzi wa magari kabla ya
kuingizwa nchini.
Sikika
inaamini kwamba TBS na TFDA ni taasisi kubwa zenye uwezo mkubwa wa
kudhibiti hali kama hii na hivyo kuhusishwa na taarifa kama hii ni sawa
na kashfa ya kushindwa kazi. Pia, TBS na TFDA wanapaswa kutoa elimu endelevu kwa watumiaji jinsi ya kutambua bidhaa bandia na halali zikiwa sokoni kabla ya matumizi.
Sikika inashauri Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii pamoja na Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko kuchukua hatua za haraka ili kuzuia mzunguko wa bidhaa zilizotajwa. Pande zote zinazaohusika ambazo hazikutekeleza wajibu wao lazima ziwajibishwe na pale inapotakikana mkondo wa sheria utumike.
Bw. Irenei Kiria Mkurugenzi Mtendaji, Sikika, S.L.P 12183 Dar es Salaam,
Simu: +255 222 666355/57, Nukushi: 2668015, Barua-pepe: info@sikika.or.tz, Tovuti: www.sikika.or.tz
Simu: +255 222 666355/57, Nukushi: 2668015, Barua-pepe: info@sikika.or.tz, Tovuti: www.sikika.or.tz
No comments:
Post a Comment