Tuesday, February 19, 2013

Kukithiri kwa uhaba wa dawa za malaria nchini



TAARIFA YA KUKITHIRI KWA UHABA WA DAWA ZA MALARIA NCHINI

29 Januari 2013

1.     UHABA WA ALu

Dawa muhimu za malaria zijulikanazo kama dawa mseto (ALu) zimeripotiwa kuadimika katika vituo vingi vya huduma za afya vya umma. Wizara ya Afya  na Ustawi wa Jamii kupitia mradi wa msonge (vertical program) unaoratibiwa na Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Malaria (NMCP) wamekuwa wakifuatilia uwepo wa dawa hizi kupitia nyenzo ya ufuatiliaji ijulinayo kama SMS for life ambayo imekuwa ikiwapa picha kamili ya hali halisi ya dawa hizi katika vituo vyote vya huduma za afya vya umma Tanzania bara. Ingawa nyenzo hii imekuwa ikitoa taarifa muhimu na kwa wakati, kuna ushahidi mdogo kwamba taarifa hizi zimekuwa zikitumika kuhakikisha vituo vya huduma za afya ambavyo vinapungukiwa ama kuishiwa ALu basi vinaletewa kwa wakati. Sikika imekuwa ikifuatilia uwepo wa ALu kwa kutumia nyenzo hii kwa takribani miaka miwili sasa na imegundua kutokuwepo kwa maendeleo yoyote. Tumeshuhudia mara moja tu mwaka jana mwezi Mei, (2012) ambapo mamlaka husika zilichukua hatua za dharura za kutatua tatizo la uhaba wa ALu katika vituo ambavyo viliripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari kutokuwa kabisa na akiba ya ALu ambapo  asilimia 37 ya vituo vilivyokuwa na uhaba kabisa ilishuka mpaka kufikia asilimia 24.

2.     TAARIFA ZA HIVI KARIBUNI ZA PROJECT YA SMS FOR LIFE

Kutokana na taarifa za hivi karibuni (28/1/2013) kupitia project ya SMS for Life, vituo 1,300 (25.59%) kati ya vituo 5,080 katika mikoa 22 Tanzania Bara vimeripotiwa kutokuwa kabisa na dawa mseto za aina zote (zero stocks).  Uhaba huu umekuwa ukitofautiana  baina ya mikoa na wilaya. Kwa mfano katika mkoa wa Dodoma, ni asilimia 3 tu ya vituo vyote vya huduma ndivyo vilivyoripotiwa kuwa na uhaba wa ALU, Singida (4%), Manyara ni (6%) na Kilimanjaro (10%) wakati katika mkoa wa Mwanza, uhaba umeripotiwa kuwa ni asilimia 57, Ruvuma (53%), Mara (46%), Kigoma (43%), Shinyanga (42%) na Tabora (41%). Hali ni tofauti kabisa kwa wilaya hususani katika mikoa yenye uhaba mkubwa. Mfano katika mkoa wa Mwanza, Wilaya ya Ukerewe imeripotiwa kuwa na uhaba wa ALu kwa asilimia 88 katika vituo vyake vya huduma, ikifuatiwa na Sengerema (80%), Geita (70%) na Misungwi (65). Hali hiii imekuwa ikijitokeza kwa kipindi kirefu sasa ingawa kumekuwa na mipango na miongozo thabiti ya kupambana na Malaria.

Sikika ilifanya utafiti (mwezi Machi, 2012 katika hospitali 54 Tanzania bara) na kubaini uhaba mkubwa wa dawa za malaria ambapo asilimia 43 ya hospitali hizo hazikuwa na dawa ya aina ya kwinini (kwa ajili ya kutibu malaria sugu) wakati asilimia 19 ya hospitali zote hazikuwa na ALu.

3.     MAAMBUKIZI YA MALARIA/VIFO VITOKANAVYO NA MALARIA

Malaria ni ugonjwa hatari na unaoongoza kwa kusababisha vifo vya watanzania wengi, hususani   akinamama wajawazito na watoto chini ya miaka mitano, hivyo upatikanaji wa dawa za malaria  ni muhimu sana katika mapambano  dhidi ya malaria pamoja na kupunguza vifo hivyo.

Maambukizi ya ugonjwa wa malaria kwa watoto chini ya miaka mitano Tanzania bara ni asilimia 18. Vituo vingi vya huduma vimekuwa vikiripoti kuwa malaria ndiyo inayoongoza kwa kusababisha vifo kwa wagonjwa wa nje pamoja na wanaolazwa ambapo zaidi ya asilimia 40 ya wagonjwa wa nje wanasumbuliwa na malaria. Hii inamaanisha kuwa watu milioni 12-16 huugua malaria kwa mwaka. NMCP inakadiria vifo vitokanavyo na malaria Tanzania kufikia 60,000 – 80,000 kwa watu wa rika zote. (Extrapolated from the under-five mortality rate in 2004-05 TDHS, size of under-five population, and the proportion of deaths attributable to malaria).

Kutokana na  takwimu za Tanzania HIV & Malaria indicator survey 2007/2008, maambukizi ya malaria baina ya mikoa, Mwanza inaonekana kuwa na maambukizi ya malaria kwa asilimia 31 ikifuatiwa na  Ruvuma (24%), Mara (30%), Kigoma (20%) na Shinyanga (30%) wakati mikoa hii ndio inayoongoza kwa kuwa na uhaba mkubwa wa dawa za malaria.

4.     FEDHA KWA AJILI YA KUZUIA NA KUTIBU MALARIA

Miradi ya kupambana na Malaria imekuwa ikifadhiliwa na wafadhili mbalimbali, hususani Global Fund, Mfuko wa ufadhili wa Raisi wa Marekani (PMI – USAID), Benki ya dunia (World Bank) pamoja na wahisani wengine. Global Fund ndiyo inatoa ufadhili mkubwa kwa asilimia 57, PMI – USAID (33%), World Bank (6%) na vyanzo vingine (4%) . Tangu 2003 mpaka 2010 malaria ilifadhiliwa kwa takribani dola za kimarekani milioni 450., Serikali kupitia NMCP ndiyo imekuwa ikiomba fedha hizi kupitia Global Fund kwa ajili ya ununuzi wa dawa za malaria, hivyo kama kunakuwa na ucheleweshwaji wa fedha kutoka Global Fund, serikali ina uwezo wa kutafuta fedha kutoka PMI ili kusaidia kupunguza uhaba wa dawa hizi. Hivyo ni jambo la kusikitisha kuona kwamba vituo vingi vya huduma vinakuwa na uhaba wa ALu.

5. MAHITAJI YA DAWA ZA ALU UKILINGANISHA NA KIWANGO KINACHOAGIZWA

Kwa wastani, matumizi ya dawa za ALu nchini Tanzania ni dozi million 1.3 kwa mwezi. Hii inamaanisha kwamba ni karibu dozi 15,600,000 kwa mwaka. Hata hivyo tukiangalia katika taarifa zinazopatikana kwenye  ripoti ya Global Fund (kupitia ripoti za AMF) tunaona kwamba kwa kipindi cha 01 Januari 2012 mpaka 17 Januari 2013 Tanzania iliagiza na kupokea dozi 4,917,780 kwa sekta ya umma kupitia Bohari Kuu ya Madawa (MSD) kwa awamu nne kwa mwaka. Wakati tunaona sekta ya binafsi iliweza kuagiza na kupokea dozi 11,527,990.

6. MAPENDEKEZO

Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Malaria (NMCP) uliopo chini ya wWizara ya Afya na Usatwi wa Jamii (MOHSW) ndio unaowajibika kusimamia shughuli zote zinazohusiana na kupambana na Malaria nchini. Mpango huu unasimamia ufadhili,  kutathmini mahitaji na kupanga ratiba za ununuzi na usambazaji. Na hivyo basi inawajibika kwa hali inayoonekana sasa ya dawa hii muhimu ya ALu katika sekta ya umma. Sikika imeona kwamba NMCP haijaonyesha juhudi zinazostahili  katika kukabiliana na upatikanaji wa dawa za ALu.

Ili kumaliza uhaba huo sugu na kuishiwa dawa mara kwa mara, Sikika inashauri kwamba MOHSW na NMCP watafute rasilimali fedha za kutosha ili waweze kununua dawa za Alu kwa kiwango kikubwa, ikibidi za mwaka mzima kwa mkupuo mmoja (dozi milioni 15.6), na kisha kuhakikisha kwamba kuna dawa za ziada za  kutosha angalau kila baada ya miezi 6. Kushindwa kutekeleza hayo kutasababisha uhaba huo kuendelea, hali ambayo itaongeza idadi ya wagonjwa pamoja na vifo vinavyotokana na malaria.

Mr. Irenei Kiria, Executive Director of Sikika, P.O.Box 12183 Dar es Salaam,
Tel: +255 222 666355/57, Cell: 0784 274039, Fax: 2668015, Email:info@sikika.or.tz,
Twitter: @sikika1, Facebook: Sikika Tanzania, Website: www.sikika.or.tz



[1] Mahitaji halisi yanaweza kuzidi  kuzidi idadi iliyotajwa, wataalamu wengine wamekadiria mahitaji halisi kuwa kati ya milioni 18 hadi 25.

No comments: