Tuesday, February 19, 2013

Wizara iache ‘siasa’ na malumbano, isambaze dawa za ALu!


TAMKO KUHUSU UHABA WA DAWA MSETO ZA KUTIBU MALARIA (ALU) –FEBRUARI 10, 2012

 Sikika imeshangazwa na taarifa za Wizara ya Afya na Ustawi waJamii kwamba kuna dawa za kutosha aina ya ALU za kutibu malaria   hapa nchini wakati ambapo vituo vya kutolea huduma vya umma vina uhaba mkubwa wa dawa aina hiyo.

Taarifa hiyo iliyotolewa na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo tarehe 1/2/2013, na kuchapishwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari ilikuwa ikikanusha tamko lilitolewa na Sikika kwenye vyombo vya habari kuhusu uhaba wa dawa mseto (ALu) kwenye vituo 1300 (26%) vya umma vya huduma za afya nchini.

Sikika  inaikumbusha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwamba kuna tofauti kubwa kati ya shehena zinazoagizwa nchini, na uwepo wa dawa hospitalini. Taarifa iliyotolewa na Sikika ilisisitiza kutokuwepo kwa dawa katika vituo vya kutolea huduma wakati taarifa ya wizara ilihusu shehena za dawa zilizoingia nchini na zinazotarajiwa kuingia.

Pamoja na Wizara kutumia nguvu na muda mwingi kukanusha uhalisia wa taarifa za uhaba wa dawa za ALu nchini,  hali halisi bado inaonyesha kuwepo ukosefu wa dawa hizo kwenye baadhi ya vituo hadi leo tarehe 10 Februari, 2013. Taarifa ambazo zinapatikana kutoka katika mtandao wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kupitia mfumo wa kielektroniki ujulikanao kama ‘SMS for life’, zinaoonesha kwamba hadi kufikia leo, asilimia 25  (vituo 1,280)  ya vituo vya afya vya umma nchini bado havina dawa zozote aina ya ALu. 

Mfumo huo pia ulionesha kwamba mikoa iliyoripotiwa na Sikika kuwa na ukosefu wa dawa (ALU na Quinine) uliokithiri hapo Januari 28, 2013 bado ilikuwa haijafikishiwa dawa zinazodaiwa kuwepo nchini. Mikoa hiyo na asilimia ya idadi ya vituo ambavyo havina dawa hizo (ALU na Quinine) katika mabano ni; Mwanza(59%), Ruvuma (49%), Shinyanga (44%), Tabora (40%), Mara (38%), na Kigoma (38%).

Kwa hali hiyo, Sikika ingependa kuamini kuwa  taarifa ya Wizara kwamba dawa za ALU zipo nchini ni za kweli. Lakini, kama taarifa hizo ni za ukweli,  kwa nini hizo dawa hazipo kwenye vituo vya kutolea huduma kwa takribani asilimia 25 kwa miezi kadhaa sasa? Je, Wizara inataka kueleza wananchi  kwamba mfumo wake wa kielektoniki (SMS for life)  hautoi takwimu za ukweli?

Taarifa ya Wizara ilidai pia kwamba  mfumo wake huo  wa kielektoniki (SMS for life), unahusika na dawa za kutibu malaria aina mbili tu ambazo ni Alu na Quinine na sio dawa nyingine za kutibu Malaria. Katika hilo, Sikika inapenda kukumbusha umma kwamba tangu mwaka 2006, Tanzania imekuwa ikifuata mwongozo wa matibabu ya malaria uliotolewa na Shirika la Afya Duniani (WHO),  unaotumia dawa ya ALu kutibu malaria ya kawaida  na Quinine kwa malaria sugu huku SP ikitumika kwa akinamama wajawazito.

Kwa mantiki hii, Sikika inaiomba Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii  kutaja hizo dawa aina zingine zinazotumika kutibu malaria ya kawaida,  ambazo hazipo katika mfumo wa ‘SMS for life’. Pia Wizara hiyo ieleze umma dawa hizo nyingine ambazo haijazitaja zinatumika kwa kufuata mwongozo upi na ulipitishwa na taasisi gani?  Je, ni lini watoa huduma walipata mafunzo ya namna ya kutumia hizo dawa aina nyingine?

Badala ya kuendeleza malumbano, Sikika inatoa rai kwa  Wizara ya Afya kuutumia vyema mfumo wake wa SMS for life kwa kujipanga ili kuhakikisha afya za watanzania zinalindwa na kwamba uhaba wa mara kwa mara wa dawa za Alu pamoja na zingine kwenye vituo vya huduma za afya, hautokei tena.

Mr. Irenei Kiria
Executive Director of Sikika, P.O.Box 12183 Dar es Salaam,
Tel: +255 222 666355/57, Fax: 2668015, Email: info@sikika.or.tz, Website: www.sikika.or.tz


No comments: