Tuesday, November 5, 2013

Tamko la Asasi za Kiraia: Mkutano wa wadau wa kutathmini sekta ya Afya


TAMKO LA ASASI ZA KIRAIA

MKUTANO WA WADAU WA KUTATHMINI SEKTA YA AFYA

Waheshimiwa Mawaziri, Katibu Mkuu, Wabunge, Mganga Mkuu, Washirika wa Maendeleo Wafanyakazi wa Wizara ya Afya, TAMISEMI, Utumishi, wawakilishi wa sekta binafsi, mabibi na mabwana, habari za asubuhi!

Tunatoa shukrani zetu za dhati kwa kupata nafasi hii kuwa watu wa mwanzo kuzungumza katika siku hii ya Sera kwa wadau wa sekta ya afya hapa Tanzania.

Sikika inasoma taarifa hii kama mwanachama hai wa Policy Forum. Policy Forum ni jumuiko la asasi za kiraia lenye wanachama wapatao 100 ambao wanalenga kuhimiza ushirikishaji wa taasisi za kiraia katika maamuzi na utekelezaji wa sera zinazomhusu mwananchi wa kawaida wa Tanzania.

Mheshimiwa Waziri, tunapenda kuanza kwa kuipongeza Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii (MoHSW) kwa kufanya tathmini ya utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Afya III (HSSP). Tumeridhika kuona kwamba taarifa ya utekelezaji wa mpango mkakati huo imeleta matokeo na mapendekezo ambayo tukiyafanyia  kazi kwa pamoja,  tunaweza kuboresha  utendaji wa sekta ya afya hapa nchini.

Tunapenda pia kupongeza sekta ya afya kwa mafanikio mengi yaliyopatikana kwa mwaka uliopita kama vile muendelezo unaofanywa wa kuimarisha mfumo wa rasilimali fedha na pia uimarishaji wa Bohari ya Dawa ya Taifa (MSD) ambao umeiwezesha kutunukiwa cheti kutoka  Shirika la Kimataifa la Viwango duniani kwa kuimarisha na kudhibiti ubora.

Mheshimiwa Waziri, licha ya juhudi zinazofanywa, bado bajeti inayotengwa kwa ajili ya sekta ya afya ni ndogo na haitoshelezi mahitaji yaliyowekwa kwenye mpango mkakati wa sekta ya afya. Bajeti ya sekta ya afya bado inategemea mno wahisani, hivyo kutishia maendeleo endelevu ya mfumo mzima wa afya.

Mabibi na mabwana, ilikuwa ni miongo miwili iliyopita, mwaka 1993, wakati serikali ilipoanzisha sera ya uchangiaji ili kuongeza rasilimali na kukuza ushirikishaji wa wananchi. Hata hivyo, watoa huduma za afya wameripoti kwetu vikwazo na changamoto wanazokumbana nazo katika kuwatambua watu wanaostahili kupata huduma za afya bure. Kwamba, nani anahusika kulipa au kufidia gharama za wanaostahili kupata matibabu bure, bado ni swali ambalo halijajibiwa.

Kuonyesha ukubwa wa hili tatizo, mathalan, asilimia 75 ya wagonjwa wote katika hospitali ya Mwananyamala wako katika daraja la watu maskini, na hivyo kustahili msamaha wa matibabu. Takwimu zilizopatikana kutoka hospitali ya Temeke zinaonyesha gharama za kutoa huduma kwa watu wenye msamaha wa gharama za matibabu zinakua mwaka hadi mwaka. Kwa mwaka wa fedha 2010/11 zilitumika dola 661,000/-, kwa 2011/12 zilitumia dola 710,000/-, na 2012/13 hospitali ilitumia kiasi cha dola 1,504,000/-. Ukilinganisha gharama hizi na uwiano wa mapato yaliyokusanywa katika miaka hiyo, ni sawa na kiasi cha dola 375,000/- kutoka kwa kila mgonjwa ambaye anaweza kulipia.

Mheshimiwa Waziri, AZAKI zinaishauri Serikali kuchukua hatua kwa kukuza na kubuni mikakati ya fedha  ambayo itajikita kuelekeza vyanzo vipya vya rasilimali kwenye sekta ya Afya. Hili linaweza kufanyika kwa kupanua wigo wa mifumo ya mfuko wa bima ya afya ya jamii, kupunguza matumizi yasiyo ya lazima na kutekeleza shughuli madhubuti zitakazoleta matokeo ya kimkakati. Zaidi, tunashauri kupitia upya mwongozo wa uchangiaji gharama ili kupunguza mzigo wa madeni kwenye gharama za uendeshaji. 

Mheshimiwa Waziri, Sikika kwa kushirikiana na Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), ilifanya utafiti ambao ulilenga katika kuangalia walipo na wanapokwenda wahitimu wa fani ya udaktari Tanzania. Matokeo ya utafiti huo yalionesha kuwa asilimia 40% ya madaktari wahitimu hawaendelei na fani ya udaktari. Na takribani 42% ya wahitimu wa fani ya udaktari wamebaki katika miji mikubwa, kwa mfano, Dar es Salaam, Arusha, Mwanza, Mbeya na Kilimanjaro. Na 32% ya madaktari wote waliohusishwa katika utafiti huu walikuwa katika Jiji la Dar es Salaam.

Kutokana na matokeo ya utafiti huu, AZAKI zinashauri mamlaka husika kuboresha mazingira yatakayowavutia madaktari na kuwafanya waendelee kuwepo na kufanya kazi katika fani yao, hasa katika maeneo ya vijijini ambayo watanzania walio wengi wanaishi.

Mheshimiwa Waziri, AZAKI zimeshuhudia changamoto nyingi za upatikanaji na uwepo wa madawa muhimu na vifaa tiba nchi nzima. Hali hii inatokana na mambo mengi kama vile upungufu wa bajeti na changamoto katika mfumo wa ugavi na usambazaji wa dawa. Kwa mfano, makadirio ya fedha zote zilizohitajika kwa ununuzi wa madawa katika mwaka wa fedha 2012/12 ulikuwa Tsh. 198 bilioni, wakati huo fedha zilizopatikana ni Tsh. 80 bilioni, sawa na 40%.  Utafiti uliofanywa na Sikika 2012 katika kuangalia uwepo na upatikanaji wa madawa na vifaa tiba muhimu katika hospitali za Serikali ulionesha kwamba 96% ya madawa yaliyotakiwa kuwepo hayakuwepo katika hospitali na 94% ya hospitali hizo hazikuwa na ama aina moja ya dawa na vifaa tiba muhimu au vyote.

Ili kuweza kukabiliana na mgawanyo huu usio sawia, ni vyema fedha zote zinazotolewa kwa ajili ya madawa na vifaa tiba zipelekwe katika vituo vya kutolea huduma kwa kuzingatia mfumo wa kukokotoa mgawanyo. Hadi sasa, bado mfumo huo wa ukokotoaji wa mgawanyo wa dawa  kulingana na mahitaji unakabiliwa na changamoto nyingi ingawa juhudi zinafanyika kuboresha taarifa na kuanza utekelezaji.

Mheshimiwa Waziri, tunaipongeza Wizara yako kwa kulifanyia kazi suala la ARV bandia zilizosambazwa katika vituo vya kutolea huduma za afya mwanzoni mwa mwaka huu. Hata hivyo, upelelezi wa polisi katika suala hili umechukua muda mrefu sana na haieleweki ni lini watuhumiwa watawajibishwa.

Mheshimiwa Waziri, wakati sekta ya afya inajikongoja katika utoaji wa mashine za kupima VVU (CD4), Shirika la Afya Duniani limependekeza utoaji wa dawa za kupunguza makali ya VVU kutolewa mapema, angalau kwa wenye CD4 500 (500 CD4 cells/mm3) badala ya kipimo cha sasa cha CD4 350 (350CD4 cells/mm3). Hii inamaanisha kwamba, watu wengi zaidi watahitaji kupima VVU na kuanza kutumia ARVs. Tunatarajia mabadiliko haya yatazingatiwa  katika mipango na makadirio ya fedha kwenye bajeti ijayo.
Mabibi na mabwana, ripoti ya ukaguzi wa fedha wa  Wizara ya Afya ya mwaka 2011/12 iliibua matatizo mbalimbali ikiwemo utunzaji mbaya wa kumbukumbu, usimamizi duni wa bajeti na mali za Wizara. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu ya Serikali (CAG) ana mamlaka kikatiba kutoa mapendekezo kwa Mhasibu wa Wizara ambaye anawajibika kulinda fedha na mali za umma. Ndio maana tunasikitika kuona kwamba, hata baada ya mwaka mmoja kupita, hoja 13 zilizoibuliwa na CAG zinazofikia kiasi cha Tsh. 71 bilioni, bado hazijafanyiwa kazi. Kufuata na kuzingatia sheria na kanuni za fedha ni muhimu ili kudumisha imani kwa wananchi katika usimamizi wa huduma za afya ya jamii.

Mheshimiwa Waziri, Asasi zinapendekeza kuwa hoja zilizoibuliwa wakati wa ukaguzi wa mahesabu  zishughulikiwe na kutatuliwa kwa haraka.

Tunaipongeza serikali ya Tanzania kwa kujiunga na Ushirikiano wa Uwazi wa Serikali (OGP)  na ahadi ilizoweka katika mpango wa utekelezaji  wa 2012-2013 ili kukuza uwazi. Pamoja na nia hiyo nzuri ,tovuti ya Wizara ya Afya bado haina taarifa nyingi muhimu hasa katika eneo la ununuzi na utaratibu wa usambazaji. Utafiti wa hivi karibuni uliofanywa na Sikika umegundua kwamba asilimia 36 ya wazabuni  wa ugavi wa aina mbalimbali za dawa kwa MSD wamelalamikia kukosekana kwa uwazi katika mchakato wa zabuni.

Tunapendekeza kwamba Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii  ianze kuweka taarifa mbalimbali za umma kwenye tovuti yake na maeneo mengine ya wazi ambapo walipa kodi na wadau wengine muhimu wanaweza kuzifikia kwa urahisi.

Mheshimiwa Waziri, uwazi katika mgawanyo wa fedha kwenye wizara bado ni suala nyeti. Katika mwaka huu wa fedha, Wizara imepanga kutumia kiasi cha shilingi 283 bilioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Takriban theluthi mbili ya kiasi hiki cha fedha kitagawanywa kwa  taasisi na Idara nje ya  Wizara kwa njia ya misaada, ruzuku, michango na mifumo mingine ya misaada. Hata hivyo, hakuna ufafanuzi wa jinsi fedha hizo zitakavyotumika.
Asasi  zinapendekeza kuwa umma upewe taarifa za ziada zinazochanganua jinsi idara na taasisi hizo zitakavyotumia fedha za walipa kodi.

Mheshimiwa Waziri, mwisho tunapendekeza ushirikishaji wa wananchi katika mipango ya afya, ufuatiliaji na usimamizi kwa kuwa kufanya hivyo ni muhimu katika kuelekea uboreshaji wa utoaji huduma za afya. Tumeshuhudia mafanikio kupitia mbinu ya ufuatiliaji wa uwajibikaji jamii ambayo inahusisha wananchi katika ufuatiliaji wa mipango ya huduma za afya, fedha na utoaji huduma katika ngazi ya wilaya. Asasi zinashauri serikali iwekeze katika mbinu za ushirikishaji jamii ili kuboresha utolewaji wa huduma za afya katika ngazi za Wilaya.

Mheshimiwa Waziri, Mabibi na Mabwana, tunawashukuru tena kwa nafasi hii ya kuhutubia  washiriki kwenye  siku hii ya Sera  na tunategemea ushirikiano wetu utaendelea kuzaa matunda kwani sote tuna mchango muhimu katika kuboresha sekta ya afya.
Asanteni!

Imewasilishwa na Bw. Irenei Kiria,
Mkurugenzi Mkuu wa Sikika, kwa niaba ya Policy Forum

No comments: